Kikosi cha wekundu wa Msimbazi, Simba kinatarajia kushuka kwenye
Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki kucheza mechi
mbili za kirafiki dhidi ya Mtibwa Sugar na moja ya timu za Ligi Kuu ya
Uganda.
Mechi hizo ni maalum kwa ajili ya kujiweka fiti kabla ya kuikabili
Yanga katika mechi ya ‘Nani Mtani 2′ itakayopigwa kwenye uwanja huo
Desemba 13.
Kocha Mkuu wa Simba, Mzambia Patrick Phiri jijini hapa leo kuwa
Ijumaa watacheza dhidi ya timu kutoka Uganda kabla ya kuwavaa wababe wa
Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara (VPL) msimu huu, Mtibwa Sugar
Jumapili.
Phiri amesema baada ya mechi dhidi ya Jumapili dhidi ya Mtibwa Sugar,
kikosi chake kitakwenda jijini Mwanza kuweka kambi maalum kwa ajili ya
Yanga.

“Tumeomba baadhi ya timu kutoka Uganda tucheze nazo kama sehemu ya
maandalizi yetu kabla ya kuikabili Yanga, bado hatujapata jibu kamili ni
timu gani ambayo iko tayari kuja lakini Ijumaa tutacheza dhidi ya timu
kutoka Uganda,” Phiri amesema.
“Jumapili tutacheza dhidi ya Mtibwa Sugar, baada ya hapo tutakwenda
kuweka kambi sehemu ambayo itajulikana baadaye lakini kwa kiasi kikubwa
tumekubaliana timu itakwenda Mwanza.”
Itakuwa mara ya pili Simba kucheza dhidi ya Mtibwa msimu huu baada ya
kutoka sare ya bao moja katika mechi yao iliyopita ya VPL iliyopigwa
kwenye Uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro.
Tangu Agosti mwaka huu, Simba imecheza mechi mbili za kirafiki dhidi
ya timu kutoka nje ya mipaka ya Tanzania tangu ikifungwa 3-0 d dhidi ya
Zesco ya Ligi Kuu ya Zambia kabla ya kufungwa 1-0 na Gor Mahia ya Ligi
Kuu ya Kenya, mechi zote zikichezwa kwenye Uwanja wa Taifa.
Simba ilishinda 3-1 katika mechi ya kwanza ya Nani Mtani Jembe dhidi
ya Yanga iliyopigwa Uwanja wa Taifa Desemba 21, mwaka jana, kipigo
ambacho kilifukuzisha benchi zima la ufundi la Yanga lililokuwa chini ya
Mholanzi Ernie Brandts, kocha msaidizi mzawa Felic Minziro (sasa Kocha
Mkuu wa JKT Ruvu) na kocha wa makipa Mkenya Razak Ssiwa.
Wengine waliotimuliwa Yanga kutokana na matokeo hayo ni pamoja na
meneja wa timu hiyo ya Wanajangwani Hafidh Saleh ambaye alirejeshwa
baadaye, hata hivyo.
Mabao ya Simba SC yalifungwa na mfungaji bora wa VPL msimu uliopita,
Tambwe aliyefunga mawili na kiungo Awadhi Juma huku bao pekee la kufutia
machozi Yanga likifungwa na Mganda Okwi ambaye amerejea tena Simba SC
baada ya kulumbana na uongozi wa Yanga SC.